Sitti Mtemvu bado kiti cha moto, mamlaka zajipanga kumpeleka mahakamani



Uamuzi mgumu wa kujivua taji la Miss Tanzania 2014, haujamaliza misukosuko inayomkabili Sitti Mtemvu. Wakala wa Uzazi, Vifo na Ufilisi (Rita) wamedai kuwa wamekamilisha upekuzi wa taarifa alizotumia kuombea cheti cha kuzaliwa na vielelezo hivyo vimepelekwa polisi.

 Ofisa mtendaji mkuu wa Rita, Phillip Saliboko na Meneja masoko na mawasiliano, Josephat Kimaro wameliambia gazeti la Mwanachi kuwa upekuzi wa nyaraka zilizotumiwa na Sitti uliofanywa na wanasheria wao, tayari umekamilika.
 “Kazi yetu (Rita) tumeimaliza na upekuzi wa taarifa za Sitti umekamilika na kinachofuata sasa ni kupeleka nyaraka hizo kwenye mamlaka inayohusika ambayo ni polisi, wao ndio wataamua nini cha kufanya,” Kimaro aliliambia gazeti hilo.
 Alisema Rita haiwezi kumhukumu moja kwa moja mrembo huyo kuwa alighushi nyaraka na kudanganya ili apate cheti hicho cha kuzaliwa kilichotolewa na Rita Septemba na badala yake wanapeleka vielelezo walivyonavyo polisi ili nao wavifanyie kazi.
 “Sisi (Rita) jukumu letu lilikuwa ni upekuzi wa nyaraka, kazi ambayo imefanywa kwa ustadi mkubwa na jopo la wanasheria wetu na hadi sasa imekamilika na kinachofuata ni kuzipeleka nyaraka hizo polisi ambao wao ndiyo wenye jukumu la uchunguzi na kumchukulia hatua Sitti au la,” alisema.

Sitti Mtemvu aliingia kwenye kashfa ya kudanganya umri wake na nyaraka zake mbalimbali zilionyesha alizaliwa 1989, umri ambao umepitiliza ule unaotakiwa kwa mshiriki wa mashindano ya Miss Tanzania, huku cheti chake kikionyesha alizaliwa 1991, hivyo kulazimika kuvua taji hilo.

Source: Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

Recent Posts