Mnara wa Kumbukumbu ya Kifo Cha Daudi Mwangosi Sehemu Ambayo Alilipukiwa na Bomu: Chadema Watoa Tamko

Waandishi wa habari Oliver Motto aliyesimama kulia ambaye ni mwandishi na mpiga picha wa Star Tv, Radio Free Africa na mmiliki wa mtandao huu, akiwa na wanahabari wenzie, aliyevaa miwani ni Reymond Fransis (Ebony Fm Radio) aliyechuchumaa ni Laurian Mkumbata ITV na Radio One wakiwa katika picha ya pamoja katika mnara huo.
Mnara wa kumbukumbu ya marehemu Daud Mwangosi, mwandishi wa habari wa Chanel Ten-mkoani Iringani aliyeuawa kwa bomu na polisi wakati mwandishi huyo akitekeleza majukumu yake ya kihabari, wakati Chadema wakizindua matawi yao ya Kata Nyololo katika Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa.

CHAMA cha demokrasia na Maendeleo Chadema kimetoa siku 30 kwa jeshi la polisi mkoani Iringa kukabidhi vyombo vya aliyekuwa mwandishi wa habari wa kituo cha Luninga cha Chanel Ten Daud Mwangosi, aliyeuawa akiwa kazini wakati wa uzinduzi wa matawi ya Chadema katika mji wa Nyololo Wilaya ya Mufindi Mkoani Iringa.

Chadema kimetoa tamko hilo katika uzinduzi wa mnara wa kumbukumbu uliojengwa Nyololo katika eneo alilouawa Daud Mwangosi siku ya tarehe 2 Septemba mwaka jana wakati akitekeleza majukumu ya kihabari.


Akizungumzia hali hiyo mkurugenzi mkuu wa chadema Taifa na aliyekuwa kamanda wa oparesheni ya M4C Benson Kigaila alisema jeshi la polisi linapaswa kujitathmini zaidi kwa kutenda haki kwa kurejesha vifaa vyote vya marehemu Daud Mwangosi kwa familia yake ili kupunguza maumivu yatokanayo na kifo hicho.

Kigaila alisema vifaa vya Mwangosi ni mali halali wala havikuwa vya wizi, kwa hiyo jeshi la Polisi halina sababu ya kuendelea kuvishikilia vifaa hivyo kwa mwaka mmoja pasipo kuvikabidhi kwa ndugu wa marehemu, kwa kuwa kufanya hivyo ni kuendelea kuitesa familia ya Mwangosi na mjane ambaye ameachiwa mzigo wa kuilea familia.

"Sioni sababu ya jeshi hili ambalo ndiyo tunaliita ni usalama wa raia na mali zao, leo hii linatimiza mwaka mmoja tangu wachukue vifaa vya marehemu Mwangosi, marehemu mpaka unamfika umauti alikuwa na vifaa vyake vyote na katika picha anaonekana akiwa ameshika kamera yake, Begi la Laptop, kuna ugumu gani wa kurudisha vyombo vyake kwa ndugu zake Mwangosi, chadema tunatoa siku 30 vifaa hivyo vyote viwe vimekabidhiwa kwa familia ya Mwangosi, maana vitu vile vilikuwa ni mali yake halali na siyo vilikuwa vya wizi, polisi wanaendelea kuvishikilia mpaka sasa vya nini kama siyo kuongeza maumivu kwa mjane na familia yake!!," Alihoji Kigaila.
 
Aidha Kigaila alisema ujenzi wa mnara huo ni kumbukumbu ya mauaji ya kikatili yaliyofanywa na polisi polisi dhidi ya mwandishi huyo, na kuwa ili kuitunza kumbukumbu hiyo mioyoni mwa watanzania, Chadema kila mwaka mbili Chadema itakuwa ikiadhimisha kumbukumbuka ya kifo hicho kama ni ishara ya kulaani mauaji ya kishenzi yaliyofanywa na polisi.

Alisema alishangazwa na jeshi la polisi kumpandisha cheo mtuhumiwa namba moja wa mauaji ya mwangosi huku baadhi ya viongozi wakimpa pongezi kwa kazi nzuri alizofanya jambo ambalo linaonyesha dhahili kuwa suala hilo lilipangwa.

"Hapa ndiyo mtaona ubia baina ya serikali, chama cha mapinduzi na jeshi la polisi, juu ya mauaji ya wananchi wasio na hatia, kumpandisha cheo muuaji hili ni jmbo la kushangaza sana juu ya serikali yetu na mpango wa kuratibu kifo cha Mwangosi, " Alisema.
 
Naibu katibu mkuu Chadema Zanzibar Hamad Mussa Yusuph alisema marehemu Mwangosi ataendelea kuwepo ndani ya mioyo ya watu duniani licha ya uwepo wa mizengwe juu ya kutaka kufuta kumbukumbu yake na kuwa kamwe chadema haitamsaliti Mwangosi.
 
Naye mchungaji Steven Kimondo mwenyekiti wa kanda ya kusini Chadema alilitaka jeshi la Polisi kuacha mara moja tabia ya kutumia nguvu kwa wananchi wasio na hatia, na badala yake nguvu hizo waelekeze kwa waharifu na watu wanaoingiza dawa za kulevya na kusababisha nguvukazi ya Taifa kudhorota.

"Ndugu zangu polisi, ninawahisi sana muache kutumia nguvu kwa raia wasio na hatia, nguvu hizo tungefurahi endapo zingeelekezwa kwa wanaoingiza dawa za kulevya nchini, majambazi na wezi wa mali za umma, lakini siyo kwa raia wema na wasio na hatia," Alisema Kimondo.

Akisoma taarifa ya ujenzi wa mnara huo wa Mwangosi katibu wa jimbo la Mufindi Kusini Emmanuel Ngwalanje alisema mnara huo wenye thamani ya shilingi Mil. 2, laki tatu na elfu ishirini umejengwa kwa ufadhili wa watanzania walioamua kuchangia mpango huo ili kudumisha kumbukumbu ya mauaji hayo.

Ngwalanje alisema kumbukumbu hiyo pia inalaani vitisho na vitendo vyote ambavyo wamekuwa wakifanyiwa wanahabari na wanaharakati mbalimbali nchini jambo ambalo linadumaza uhuru wa habari.

"Hii ni ishara ya kulaani ukatili, vitisho na vitendo vyote wanavyofanyiwa waandishi wa habari pindi wanapotaka kufanya kazi zao za kihabari, kwani kumekuwa na matukio mengi yanayoendana na hili la Mwangosi kama Richard Masatu wa gazeti la Kasi mpya maiti yake iliokotwa katika eneo la Igoma jijini Mwanza akiwa ametolewa macho huku mguu wa kushoto na mbavu zikiwa zimevunjwa, naye mwandishi Issa mwandishi wa redio Kwizela aliuawa na maiti yake kuokotwa katika poli la kilima Kajuruheta katika kijiji cha Mhange Wilaya ya Kakonko mkoani Kigoma ambapo inadaiwa mwandishi huyu alinyongwa na kisha kupigwa risasi hii ni hatari sana tusipopaza sauti watanzania," Alisema.

Aidha alisema pia siku za hivi karibuni mhariri mtendaji wa New Habari Media Group Absalom Kibanda alitekwa, akateswa kwa vipigo, akakatwa kidole cha mkono wa kulia, kutobolewa jicho la kushoto, kung'olewa meno, kucha na kisha kutupwa nje ya lango la nyumba yake Mbezi Beach ni kati ya mambo yanayoendelea na kamwe wao hawatayafumbia macho.

Frenk Nyalusi ambaye ni mjumbe wa kamati tendaji Chadema wilaya Iringa alisema Mwangosi hakufa kwa mapenzi ya Mungu bali kwa mipango ya binadamu na kamwe hawatakubali kuyafumbia macho matukio ya unyanyasaji yanayofanywa kwa uratibu wa baadhi ya viongozi wa serikali.

"Siku tunayokuja hapa Nyololo tukiwa mjini tayari tulishakuwa tumepata taarifa kuwa polisi wamejipanga kufanya tukio la mauaji, na haikujulikana wamemlenga nani, lakini niseme ndugu zangu, kama hatutasimama na kupaza sauti kukemea matukio haya tujue wote tutaangamizwa, kwani hata Mwangosi hakufa kwa mpango wa Mungu, ni masuala yaliyokuwa yamepangwa," Alisema.


Akizungumzia juu ya ujenzi wa mnara huo ulioleta utata kwa baadhi ya wanahabari na Chadema, Andrew Mogella Mwangosi ambaye ni mdogo wa Mwangosi na msemaji wa familia hiyo alisema mnara huo umejengwa kwa ushirikiano kati ya familia yao na Chadema, kutokana na kifo cha ndugu yao kutokea katika kazi ya chama hicho.

Andrew alisema dhamana ya Mwangosi ipo mikononi mwa wanafamilia yao, na baada ya kuona umuhimu wa shughuli ya ujenzi wa mnara huo walikubaliana ili eneo hilo liwe Kaburi la kwanza la Mwangosi, huku kule kijijini Tukuyu ulikozikwa mwili wa mwandishi huyo likiwa ni kaburi la pili.

"Daud Mwangosi alikuwa kaka yangu, na tulikuwa wawili tu, sasa nimebaki pekeyangu katika uzao wa mama, ninajisikia uchungu mkubwa kusimama hapa, nimesikia maneno mengi juu ya ujenzi wa mnara huu, ninaomba niseme kuwa tangu awali mpaka sasa familia imeshirikiana vyema na Chadema, niwaombe ndugu zangu waandishi ambao mmekuwa mkiandika habari za kupotosha acheni, ninajua baadhi yenu mna maslahi binafsi, ninathamini sana mchango ni ushirikiano wenu mliotuonyesha tangu kifo cha kaka yangu mpaka sasa, lakini acheni kuingilia masula ya familia kwa kuzungumza masuala yasiyofaa, mnatuumiza sasa, kaka yangu aliuawa wakati akiwa katika kazi yake ya habari kwenye shughuli za Chadema, ninawaomba mtambue hivyo na siyo kingine, ninawaombeni Chadema mpuuze maneno ya baadhi ya wanahabari wenye maslahi yao binafsi," Alisema.


Hatua hiyo imekuja baada ya uwepo wa malumbano makubwa ya ujenzi wa mnara huo kutokana na baadhi ya wanahabari wakipinga suala hilo, kwa madai kuwa linaongozwa kisiasa, huku familia ikisema kuwa mnara huo ni kaburi la kwanza la Mwangosi na lile la Tukuyu ulikozikwa mwili wake likiwa ni kaburi la pili, na kuwa eneo hilo kwa ujirani litawafanya ndugu na watoto wa marehemu kufika kwa urahisi.

Mareheme Daud Mwangosi aliuawa na askari polisi Septemba 2 kwa kulipuliwa na Bomu katika eneo hilo la nyololo wakati akiendelea na kazi zake za habari, baada ya jeshi la polisi kupinga shughuli za uzinduzi wa matawi ya Chadema, hata hivyo wananchi bado walikuwa na uoga wa kufika katika eneo la tukio la uzinduzi wa mnara huo, ni baada ya kuona idadi kubwa ya askari Polisi, hatua iliyowafanya Chadema kuwataka polisi wenyewe kutangaza uwepo wa shughuli hizo ambazo zilifuatiwa na mkutano wa amani, huku baadhi ya wananchi na viongozi walioshuhudia tukio hilo wakiangua vilio.

Recent Posts